Saturday 8 October 2016

UKITAKA KUMFUGA CHATU, UANDAE UNGA WA KUMLISHA

Hii ni makala yangu  iliyotolewa leo Oktoba 8, 2016 kwenye gazeti la TanzaniaDaima, kama hukupata nakala yako na kwa kukujali msomaji wa petermmbaga.blogspot.com isome hapa kwa utulivu.



Na
PETER MMBAGA, UDSM(SJMC)

“Ukitaka kumfuga chatu, uandae unga wa kumlisha”  hiyo ni kauli ya “kijana wa zamani”   kwenye kijiwe kimoja nikiwa kwenye harakati za kumng’ojea mgeni  wangu kituo cha daladala  mida ya jioni baada ya jua  kunipiga vilivyo mchana wake, nikamuuliza “kijana wa zamani” unamaanisha nini?
Akanambia kijana huelewi nini? Mimi nina elimu ya mkoloni nayo inanipa nguvu kudadavuadavua  yaliyomo kidogo, Je, wewe vipi?
Nikamwambia nijibu basi  “mzee kijana” akasema “homu weki” hiyo, wakati natafakari kabla  mzee hajatoa hoja ya msingi juu ya maana ya msemo wake, ndipo stori kijiweni zikazidi kunoga, kuna mshikaji moja akazungumza kuhusu  UKUTA(akimaanisha operesheni ya  CHADEMA) aliyotakiwa kufanyika septemba mosi ikasogezwa tena oktoba mosi kisha kuahirishwa kwa mara nyingine.
Jamaa mmoja akadai hawa  maCHADEMA nao wamezidi kila kitu wanahisi wanaonewa, mwacheni  ndugu Magu(Rais John Magufuli) apige kazi bwana! Mzee tunayemwita “mzee wa busara”  akajibu hii ni kizungumkuti kila mtu anavutia kwake ila serikali iwe makini kwa kauli ya rais kusema hakuna siasa  mpaka 2020, sasa kazi ya vyama vya siasa ni nini?
Kuna mvutano wa CUF na Profesa Ibrahimu  Lipumba  nikawa nawaza kichwani mwangu wakati huohuo kuna mbasi akaja na akatusikilizisha sauti  ya Rais JPM juu ya kuhamia Dodoma. Kwa hisia kidogo akataja kuwa haiwezekani baba wa Taifa mwalimu Nyerere alisema makao makuu ni Dodoma hivyo kupinga”.
Mzee anayeuza kahawa akasema naona mmedakwa na kuhamia Dodoma, Yule mleta hadithi za Dodoma akasema “Bongo iliitwa Tanzania kila kitu kilipatikana hapa, get ready with dom” akatia na umombo  kwa mbwembwe kidogo, tukacheka sana!
Uchumi wa Tanzania, au uwepo wa Tanzania unahitaji kutegemeana ili kumvusha mama Tanzania kwenye lindi la umaskini, sasa wakati ninawaza hilo mulemule jamaa mmoja akasema “mgawanyiko wa kiuchumi na kiutendaji unabidi uguse nchi nzima”, serikali si inahama yote bwana!
Tukashindwa kuelewa anamaanisha nini? Akasema ule mlundikano wa wizara hapa Dar, au ukipita mtaa wa Magogoni unaona nini? Tukashangaa, nikamuuliza kwani tatizo ni nini?
Akanijibu “Mbasi nawe unaonekana huoni mbali, mimi naona tugawe wizara hata kimkoa  au kikanda hivi kama Arusha ndiyo kitivo cha utalii Tanzania, ni vema Wizara hata ikawa pale, haya maswala ya bandari na usafirishaji wa maji ukaa “centre” ya mikoa husika kama Dar, Tanga na Mtwara”
Mzee mkongwe akasema ni wazo zuri lakini mbona kwenye ofisi za mkoa ama wizara, ofisi ndogo za mkoa zipo hizo ofisi hata nchi zilizoendelea sidhani kama zina kitu kama hicho! Mbasi mmoja akasema hiyo haitoshi ila ili kuweka mgawanyo wa kiserikali, ili “decentralization” ya serikali za mitaa mpaka serikali kuu hawafiki vyema, hii ni sera ya kibunifu!

Mzee kijana akasema enzi hizo kwenye historia  ya utawala wa Mwingireza  kama vijana mnasoma,  Idara za serikali zilikuwa hazipo mikoani na wakuu wa Idara hawakutaka kuhama Dar, mchakato wa kupata sehemu tulivu ya mji mkuu mpaka kufika mwishoni mwa mwaka 1920, Idara ya kilimo na ofisi ya mkuu wa mkoa wa Mashariki zilihamia Morogoro, Idara ya mifugo ilikwenda Mpwapwa sasa je, kwa mgawanyo huo tu wa kipindi hicho wizara haziwezekani kweli? Tukajiumauma tukijibu “inawezekana mzee, eeh inawezakana mzee ila kwa mipango”
Kuna jamaa akatoa nje mada kidogo akadai “ving’ora viletavyo foleni vitapungua jijini bora waende dom”, tukamshangaa nikajiuliza hivi foleni Dar kumbe inachangiwa na misafara ya hawa waheshimiwa, nikacheka kidogo!
Wakati kahawa inaendelea kuchemshwa mzee wa kahawa akasema “nasikia wakuu wanaharakisha uboreshwaji wa hadhi ya kimataifa  hata kwa viwanja vya ndege Dodoma kurahisisha usafiri na hata mdege  umeshuka juzi toka Kanada”,  kuna mfanyakazi mmoja wa benki akadai mbona ukarabati wa  uwanja Dar unafanyika pia, hapo hakuna hoja labda useme fursa gani zimekwepo baada ya uwepo wa uwanja mkubwa wa Dar, ajira zimetoka na zitakazotoka kwa upanuzi unaoendelea.
Jamaa mmoja akanena “hapa Bongo hawajapaendeleza kivile, nadhani wangepaendeleza Dodoma vyema na nchi kiujumla hata kama wazo ni la tangu uhuru kuhusu kuhama, je, mikakati waliyoanza nayo kwa awamu zilizopita ikoje? Nikamjibu  jibu la swali kwa swali “kuhusu miundombinu kiujumla eeeh?”
Yule jamaa wa benki akamjibu “umefanya utafiti kuwa hawajajiandaa vyema, utafiti mbele ndipo ukosoe”, akabaki tunashangaa, asijue la kujibu!
Nikamuuliza mzee kahawa vipi? Akajibu piga domo kwanza, ndipo nikauliza hivi huo uchumi mnaozungumzia mipango miji inaridhishaje? Mzee wa kahawa akadakia akasema walicho “bugi” muda mrefu Dar haikuwa na mipango miji, na mimi nkamropokea “kazania kahawa wewe”
Mshikaji mmoja akajibu “mzee kaongea bonge la hoja wewe, mipango mikakati hamna jiulize wazo dogo la kujenga hata “hoteli” ya nyota kadhaa pale jirani na uwanja wa ndege wa J.K Nyerere  ili kupambana na ajira, pato la taifa, foleni  pamoja na muda kwa wasafiri  hilo haliwaziki kabisa, hii ndio Tanzania”
Aliposema foleni nikamkumbuka mbasi wangu mmoja aliyenieleza habari za semina moja aliyohudhuria katika hoteli ya Blue Pearl, moja kati ya wasemaji wa hiyo semina alizungumzia hali ya foleni ya Bongo aliyodai inavyosikitisha kwani haiwezekani atoke Afrika kusini kuja Tanzania kwa masaa matatu na kutoka uwanja wa ndege J.K Nyerere mpaka Blue Pearl kwa masaa hayohayo matatu, akastaajabu! Ila sisi hatukustaajabu ndio huku “kwetu” kulivyo!
Mzee wa busara akasema nasikitika  pale “nkulu” akimaanisha Ikulu, hata mashujaa wetu hawathaminiwi hata kwa kumbukumbu angalia, anwani ya nkulu wanaandika barabara ya “Barack Obama” hivi hata kuiita bararaba  ya  Mangi Marealle, Kinjekitie Ngwale au Mirambo. Kuna jamaa muuza chips jirani kwanye kibanda kilichoandikwa  “Hapa Kazi Tu chips” akasema  wakihamia kuna barabara inaweza kuitwa  barabara ya “George Bush”.  Nikamjibu kwa mbwembwe za kimombo “are you serious”. Akanijibu hapa Dar mbona imewezekana?
Kahawa ikawa tayari tukaanza kunywa uchungu wa kichangamsha mwili kile,  ndipo jamaa yetu wa bodaboda akatokea akisema  hii hela kutonekana mwisho wake ni nini?  “Mzee kijana”  akadakia akisema kila sehemu hakuna hela halafu eti majipu yametumbuliwa pesa iko wapi?
Yule jamaa wa benki akasema kwenye uchumi kuna kitu kinaitwa “economic paradoxes”, naona mnashangaa sana uongozi uliopita kulikuwa na ufisadi, na rushwa  na bado pesa ilikwepo lakini sasa hivi hela hamna mnasikia majipu yametumbuliwa mengi.



Mawasiliano kwa namba 0656 859045 au barua pepe petermmbaga29@gmail.com

Sunday 2 October 2016

DAR DERBY SIO SEHEMU YA KUCHEZEA HISIA ZA WATU

Na
Gilbert Nchimbi, SJMC
+255 657 215 404

Mpira wa miguu ni mchezo unaopendwa na watu wengi sana duniani kwa hapa Tanzania, klabu kubwa za Simba na Yanga zina mashabiki wengi mno ndio maana uwanja unajaa sana zikikutana.

Hawa  watu wakikusanyika pale Uwanja wa taifa sio kama kuna sehemu wanalipwa, sio kama wanakodiwa mabasi kwenda kwenye ule mkusanyiko kama ambavyo tumezoea kuona kwenye mikutano ya siasa, mara huyu kapewa fulana huyu kapewa khanga,  huyu kapewa kofia,  huyu kakodiwa basi ili afike kwenye mkutano lakini kwenye mpira ni tofauti wale watu uliowaona pale uwanja wa taifa kushuhudia pambano la simba na yanga hawajakodiwa gari jumamosi ya jana  wala hawalipwi kufika kuona ile mechi cha zaidi wale ndio huwa wanalipa pesa zao kuingia pale uwanjani yaani kinachowapeleka pale ni mapenzi na hisia zao walizonazo juu ya timu zao watu wanazipenda hizi timu watu wanapoteza fahamu kwa ajili ya hizi timu watu wamepoteza maisha sababu ya Simba na Yanga.

Sasa mnavyoleta masihara na hisia za watu wale pale uwanjani kwa kutuwekea marefarii ambao wanashindwa kusimamia sheria kumi na saba za huu mchezo wa soka kuna hatarisha sana maisha ya wapenzi wa huu mchezo tuwe makini na waamuzi makosa yao yanapelekea amani kuvurugika uwanjani watu wanashindwa kuvumilia zingatieni sana huu mchezo mpira wa miguu ni zaidi ya mchezo,  mpira wa miguu ni maisha watu wanahitaji haki itendeke ili waishi kwa amani. Ni zaidi viti mia mbili kuharibiwa na baadhi ya watu kujeruhiwa hiyo jana.

Tusitake yanayotokeaga kwenye mechi za watani wa jadi kwenye nchi za wenzetu yatokee nchini kwetu ndo tuanze kulizingatia hili.