Saturday 15 October 2016

TCRA YAWATAKA MAWAKALA WASIINGIZE BIDHAA ZA SAMSUNG NOTE 7

Mamlaka ya wawasiliano Tanzania (TCRA) imewataka wafanyabiashara wenye leseni za kuingiza simu nchini, zinazotolewa na mamlaka hiyo, kutekeleza maagizo yaliyotolewa na Kampuni ya Samsung ya kurejesha simu za kisasa za Samsung Galaxy Note 7 baada ya kubainika zina matatizo ya betri. Akizungumza Dar es Salaam Ijumaa hii na gazeti la habari leo, meneja mawasiliano wa TCRA, Innocent Mungy, alisema ni vyema mawakala hao wakatekeleza maagizo hayo, kwani simu hizo ni hatari kuendelea kutumika.

“Simu hiyo tayari Samsung wenyewe wamesema ina matatizo ya betri na mara mbili sasa imelipuka, hakuna faida ya mtu kuendelea kuitumia unaweza ukasababisha hatari kubwa, inapolipuka inaweza kukuondoa mikono, inaweza kulipua nyumba na matatizo mengine tunawataka wenye simu hizo kuziridisha haraka,” alisema Mungy.
“Taarifa tulizonazo haijaingia sana hapa nchini lakini wapo walioletewa kama zawadi kutoka nje ya nchi nawaomba warudishe huko kuepuka matatizo yanayoweza kujitokeza,” aliongeza.
Samsung iliwataka watu waliokuwa wamenunua jumla ya simu milioni 2.5 mwezi Septemba mwaka huu, kuzirejesha madukani baada ya wateja wengi kulalamika kwamba betri za simu hizo zilikuwa zinalipuka. Katika hatua nyingine, wiki iliyopita, Kampuni hiyo ya Samsung ya Korea Kusini ilitangaza kuwa imesitisha utengenezaji wa simu aina ya Galaxy Note 7.

Aidha Mungy aliwataka wananchi ambao tayari wanatumia simu hizo kuzizima na kuzirudisha haraka katika maduka walikozinunua ili kuepusha hatari ambayo tayari Samsung wameshaitoa.


No comments:

Post a Comment